Hata kwa ng'ombe 100 bado kwa umri ni Mtoto
Na.MED News.
Safari ya Tumaini Msowoya katika kubaini changamoto za Elimu kwa wasichana katika Halmashauri ya Wilaya ya Bahi Mkoani Dodoma inakutana na vigingi vya aina yake. Hakati tamaa; bado ana matumaini makubwa ya kufanikiwa. Tumaini Msowoya, Mwananchi tmsowoya@mwananchi.co.tz
Kwa ufupi
“Sisi tulichokitaka ni mwanamke, tulimpa baba yake ng’ombe
30 tukamchukua, hivyo huyu siyo mtoto ni mkubwa tu.” Ilikuwa sauti ya mwanamke aliyekuwa ameongozana na wasichana
wawili ambao kwa makadirio mmoja ana umri wa miaka kati ya 13 na 14 na mwingine
15 au 16.
Nilikutana nao katika Kijiji cha Chikola, Tarafa ya Chipanga
wakati nikienda kwenye kata za Chali na Chifutuka zilizopo umbali wa takriban
kilometa 120 kutoka makao makuu ya Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma. Baadaye nilikuja kubaini kwamba wasichana hao walikuwa
wakifuata ng’ombe malishoni.
![](https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEgyo2MOZ8PQgKkO7ye1aw-9YJMNPCBj8-2WR9OIBl2vGsuueREWTt0Xpc5voIFyieCBdoJrDN8tzj_mjNmOKpK-66oTtO1k1QcIyfzm8xPe2IWa85FKZtmXHT-OVeYQj2tlj1S_69DBuSEY/s320/IMG_20170803_120706.jpg)
Niliwaamkia mara ya pili bila majibu, niliamua kuwageukia
mabinti. “Hamjambo watoto wazuri?” Walinijibu: “Hatujambo, shikamoo”.
Ghafla mama yule aliyekuwa nao aliingilia kati. “Huyu siyo mtoto ni mkubwa labda huyu mwingine, yeye ndiyo
mtoto,” alisema huku akionyesha kwa kidole, yupi mtoto na yupi mkubwa kati ya
mabinti wale wawili.
Majibu yake yalinipa hamu ya kutaka kujua zaidi kulikoni
msichana anayeonekana kuwa ni mtoto aitwe mkubwa? Nilijiuliza, mbona mimi
namuona kama mtoto? Niling’ang’ania kujua kwanini anamuita mtoto ni mkubwa, baadaye mama yule aliweka wazi akisema: “Huyu ameshaolewa
tena kwa sherehe. Ni mkubwa sasa.”
Nilimtazama kwa makini msichana huyo aliyejitambulisha kwa
jina la Mage Kayungilo, nikabaini kwamba tumbo lake ni kubwa, hivyo nilihisi
kwamba ni mjamzito. Nikawaza, kumbe mtoto huyu anakabiliwa na majukumu ya ndoa.
Mwanamke aliyekuwa ameongozana naye ni mama mkwe wake.
“Kijana wangu alimpenda, amemuoa na sasa wanaishi wote,”
anasema mama huyo ambaye hakutaka kabisa kutaja jina lake. Binti huyo alitakiwa kuwa kidato cha kwanza mwaka huu, kwani
alihitimu darasa la saba mwaka jana katika Shule ya Msingi Chiguluka na kufaulu
kuingia kidato cha kwanza. Hata hivyo hakwenda sekondari na badala yake
aliolewa.
Mage anasema: “Harusi yangu ilikuwa mwaka huu, ilikuwa nzuri
na tulikula wali. Ila napenda sana kusoma.”Awali ilikuwa vigumu kuzungumza na binti huyo kwani alikataa
hata kutaja jina lake na shule aliyosoma, lakini kadri mazungumzo yetu
yalivyoendelea alikubali kuzungumza.
Baada ya kama dakika kumi za kuzungumza nao, waliamua
kuondoka, nami nikaendelea na safari yangu. Mage kwa umri wake ambao ni kati ya
miaka 14 na 15 hivi, alipaswa kuwa darasani kwani alifaulu mtihani wa darasa la
saba na kuchaguliwa kwenda kidato cha kwanza.
Ushauri
Sheria
![](https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEhWIfZLcBw9W9K-lCD_E3BaGsklCQExNmdX5lLsqTv9ZEAX0HPBh-P2adJfxlvZTXGiCs4vH0dAr9EWvTehyP4VRLPzyNACBdY7ezmU9Y_RDRODy93J3my6Vxn3xlF6JcJJ4QSi0nI4eajJ/s320/IMG_20170804_094020.jpg)
Kwa upande wa kifungu cha 60A (5) kinatoa fursa kwa vifungu
vilivyoko kwenye kanuni za adhabu (penal code) vinavyohusiana na makosa ya
kujamiiana kwa watoto wenye umri chini ya miaka 18 pamoja na makosa yanayotajwa
kwenye Sheria ya Mtoto ya 2009, kutoa adhabu sambamba na Sheria ya Elimu ikiwa
kesi inamuhusisha mwanafunzi mwenye umri chini ya miaka 18.
Takwimu za afya na idadi ya watu nchini za 2016 zinaonyesha
kuwa Mkoa wa Dodoma unashika nafasi ya nne kwa mimba za utotoni ukiwa na
asilimia 51, nyuma ya ShinyanGa (asilimia 59), Tabora (58) na Mara 55.
Taasisi ya kimataifa ya Haki za Binadamu iitwayo Human Right
Watch, katika ripoti yake iitwayo, ‘Nilikua na Ndoto ya Kumaliza Shule:
Changamoto za Elimu ya Sekondari Tanzania’, inasema katika kila watoto watano
wa kike nchini, wawili huolewa kabla ya miaka 18. Wilayani Bahi, Mwananchi liliambiwa kuwa ndoa za utotoni
zimekuwa zikifungwa kwa siri, zikiwahusisha wanafunzi ambao hukatisha masomo.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Makanda, Chonama Sekondari anasema
udhibiti wa ndoa hizo unahitaji nguvu za ziada. “Ingekuwa wanafanya hadharani
tungeweza kuwakamata, hivi juzi tu tulisika kuna harusi inaandaliwa, walipojua
tumejua, wamesambaratika,” anasema.
Kauli yake inaungwa mkono na ile ya Mwenyekiti wa Kijiji cha
Bahi Sokoni, Macheti Mlyanzoka ambaye anakiri kwamba ndoa za utotoni zipo hata
kwenye kijiji chake na zinafungwa kwa siri.
“Hii ni changamoto kubwa na kinachoumiza ni kwamba
zinafungwa kwa siri,” anasema. Mwenyekiti huyo anataja Kitongoji cha Sanduli
kuwa kinaongoza kwa ndoa za utotoni kati ya vitongoji 18 vya kijiji hicho.
“Mtaa wa Sanduli ndiyo wenye ndoa za utotoni zaidi, wazazi
wanachotaka ni mahari tu na wakishaona wana watoto wa kike na wamekua huanza
kuwarubuni waachane na masomo. Wanaamini mtoto wa kike ni mtaji,” anasema. Maneno ya mwenyekiti huyo yanashabihiana na yale ya mwanamke
aliyekuwa na mabinti wawili, akijisifu kwamba walilipa ng’ombe 30 na kumchukua
binti.
Afisa Mtendaji wa Kata ya Chifutuka, Gasper Mhembano
anasema: “Wanajua sheria haipo upande wao ndiyo maana hawazitangazi, sherehe
zao wanafanya kwa siri na wanaotusumbua zaidi ni jamii ya wafugaji.” Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Chifuduka, Daniel Mchomvu
anathibitisha kwamba ameshakutana na kesi za wazazi kuwabembeleza watoto wao wa
kike wakatae shule, lakini akasema tatizo ni usiri uliogubika vitendo hivyo.
Wasichana wafichwa
“Tumewaweka mahali wasikokutana na wazazi wao mpaka
watakapomaliza mitihani,” anasema na kuongeza: “Tuna hakika watafaulu na
watafaulu tu, sheria inawabana wazazi kuhakikisha wanaendelea kuwasomesha.” Anasema hatua ya kuwahifadhi ni kuwatenga na wazazi ambao
wamekuwa wakiwashawishi wasizingatie kwenye mitihani ili waachane na masomo.
Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Chikopelo, Cornelius Mahinyila
anasema ndoa za utotoni zipo japo wengi wanaoolewa ni wale walioacha shule au
kutoanza kidato cha kwanza licha ya kufaulu.
“Kuna msemo wazazi huwa wanawaambia watoto wao ‘nenda
kayakoroge’ ili wakiacha shule na kurudi nyumbani aolewe,” anasema. Mwalimu wa Taaluma wa Shule ya Sekondari Magaga, Jaliwa
Mahenge anasema mipango ya kuacha shule hupangwa kati ya wazazi na wanafunzi.
Kaimu Ofisa Elimu Taaluma wa Shule ya Msingi wilayani Bahi,
Grace Samwel anasema matajiri wa ng’ombe ni miongoni mwa watu hatari kwa watoto
wa kike. “Mtoto wa kike anaweza kuwa na uwezo mzuri darasani, tajiri
ng’ombe akamrubuni anaacha shule baadaye anaolewa huko,” anasema.
Anasema mwamko mdogo kuhusu elimu hasa kwa mtoto wa kike
ndiyo unaosababisha watoto wa kike kuolewa kwenye umri mdogo.
ATOA NG'OMBE 30 ILI AOZWE MWANAFUNZI
Reviewed by Unknown
on
November 21, 2017
Rating:
![ATOA NG'OMBE 30 ILI AOZWE MWANAFUNZI](https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEgyo2MOZ8PQgKkO7ye1aw-9YJMNPCBj8-2WR9OIBl2vGsuueREWTt0Xpc5voIFyieCBdoJrDN8tzj_mjNmOKpK-66oTtO1k1QcIyfzm8xPe2IWa85FKZtmXHT-OVeYQj2tlj1S_69DBuSEY/s72-c/IMG_20170803_120706.jpg)
No comments: